12/05/2026
:
Jeshi la Polisi Mkoa wa Kilimanjaro linamsaka mtu mmoja aitwaye John Anselim Filipi kwa kosa la kumjeruhi Thomas Filipi Silayo (75), mkazi wa Mbomai Tarakea kwa kumkata na kitu chenye ncha kali miguuni, tumboni na mkononi.
Akizungumza na vyombo vya habari Mjini Moshi,Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro (SACP) Simon Maigwa amesema kuwa tukio hilo lilitokea Mei 8, 2026 majira ya mchana huko kijiji cha Wama, Kata ya Ubetu Kahe, Tarafa ya Usseri, Wilaya ya Rombo, Mkoa wa Kilimanjaro ambapo mtuhumiwa huyo alimshambulia kwa kumkata na kitu chenye ncha kali baba yake mkubwa aitwaye Thomas Filipi Silayo wakati akishugulikia mgogoro wa mipaka ya shamba la familia na kupelekea majeraha makubwa kisha mhalifu huyo kukimbia kusikojulikana.
Amesema kuwa Majeruhi huyo alipatiwa huduma ya kwanza hospitali ya Wilaya ya Rombo Huruma na baadaye alikimbizwa Hospitali ya Rufaa KCMC Moshi ambako alifariki dunia akiwa anapatiwa matibabu Mei 9, 2026.
"Jeshi la Polisi Mkoa wa Kilimanjaro linawasihi Wananchi kutoa taarifa zitakazosaidia kumpata mtuhumiwa huyo ili achukuliwe hatua za kisheria" alisema Kamanda Maigwa.