
17/03/2025
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imeishauri Serikali kutafuta fedha za kuwalipa fidia wananchi waliopitiwa na Miradi ya kufua Umeme ya Ruhudji na Rumakali, ili wananchi hao wapishe maeneo hayo na waweze kuendelea na shughuli zao za kila siku wakati miradi hiyo ikisubiri kutekelezwa.
Kauli hiyo imetolewa na Mwenyekiti wa Kamati hiyo, ambaye ni Mbunge wa Same Mhe. David Mathayo baada ya kupokea taarifa ya utekelezaji wa miradi ya umeme katika Mkoa wa Njombe, tarehe 16 Machi 2025.
Mhe. Mathayo amesema, Serikali itafute fedha za kuwalipa fidia wananchi walioathiriwa na miradi hiyo ili wananchi hao wapishe na meneo hayo na waendelee na shughuli zao zingine wakati serikali ikiendelea kutafuta fedha za kutekeleza miradi hiyo.
“ Tayari tathmini imeshafanyika kwa wananchi watakaopitiwa na mradi huo na gharama za kuwalipa zimefahamika,na wananchi wanayo hiyo taarifa, ni vyema sasa serikali ikatafuta fedha za kuwalipa fidia wananchi hao ili wakaendelee na Maisha yao mengine wakati juhudi za kutekeleza mradi hiyo zikiendelea kufanyika”, alisisitiza Mhe. Mathayo.
Kwa upande wake Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Judith Kapinga, akizungumza kwa niaba ya Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko, amesema Wizara ya Nishati pamoja na Taasisi zilizo chini yake wamepokea maelekezo ya kamati hiyo pamoja na shukrani kwa niaba ya serikali, katika kutekeleza miradi ya umeme.
Kuhusu suala la fidia amesema kuwa Serikali imekuwa ikilipa fidia kwa wananchi wote wanaopisha miradi mbalimbali inayoanzishwa nchini, ikiwemo hiyo ya Ruhudji na Rumakali yenye thamani ya shilingi Bilioni 63.
Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini REA, Mhandisi Jones Olotu amesema kuwa mwambao wa Ziwa Nyasa una maeneo korofi ambayo hayafikiki kirahisi katika utekelezaji wa mradi wa usambazaji umeme vijijini kwa kuwa hakuna miundombinu ya Barabara na kuahidi kutafuta utaratibu maalum wa kumpata mkandarasi mahsusi wa kutekeleza kazi hiyo ambapo sasa kazi kufanya upembuzi yakinifu inaendelea .