
27/07/2025
HAPA SIMBA SC MMEBUGI SANA | BAADAYE MSIANZE KULAUMU
Kupitia ukurasa rasmi wa Instagram wa Singida Black Stars, taarifa imetolewa kuwa Jonathan Sowah amesajiliwa rasmi na Simba SC. Mwanzoni, hizi zilionekana k**a tetesi zisizo na mashiko — lakini sasa ni rasmi. Hili, kwangu binafsi, si jambo la kushangaza.
Soka ni k**a siasa. Hakuna adui wa kudumu, wala rafiki wa kudumu. Lakini kuna baadhi ya matukio yanayozua maswali ya msingi.
Kabla ya kujiunga na Singida Black Stars, Sowah alipokuwa Medeama, alionekana wazi kuwa na mapenzi na heshima kubwa kwa Yanga SC. Aliposajiliwa na Singida, bado alikuwa na uhusiano wa karibu na miamba hao wa Jangwani. Hakuficha mapenzi yake kwa Yanga — hata Rais wa Yanga, Injinia Hersi Said, alionekana kumwelewa na kumkubali.
Lakini leo, Sowah kasaini Simba SC. Swali ni, nini kilitokea kati ya Sowah na Hersi? Walikoseana wapi? Ni mazungumzo gani yalivunjika? Mambo haya hayapo wazi, lakini tunajua moja — mpango wa kumsajili Sowah Yanga umezimika, na Simba wamechukua nafasi hiyo.
Kumbuka: Huyu ni mchezaji ambaye alijiunga na Singida dirisha dogo la usajili, akasaidia timu hiyo kufuzu hadi Nusu Fainali ya CRDB Federation Cup, na pia akaipeleka Simba nje ya mashindano hayo! Leo hii huyo huyo amejiunga na Simba. Ajabu, siyo?
Inasemekana usajili huu umefanywa kwa ushawishi wa Mlezi wa Singida Black Stars, Mwigulu Nchemba, na Rais wa Simba, Mohamed Dewji. Je, hili ni tukio la mpango maalum au dili lililotengenezwa chini ya meza?
Wapo wanaosema kuwa Sowah ni chaguo la Kocha Fadlu Davids. K**a ni kweli, basi Fadlu anaamini anaweza kumrekebisha kiutendaji na kimaadili. Lakini je, Sowah ataweza kuendana na utamaduni wa soka la Kibongo? Ataweza kuhimili presha ya mashabiki, vyombo vya habari, na mahasimu wa jadi?
Tusisahau, kuna madai ya muda mrefu kwamba baadhi ya wachezaji hujihusisha na michezo ya kupanga matokeo — kuuza mechi! Siwezi kusema hili linamhusu Sowah, lakini kila tetesi ina chanzo chake. Wasiwasi ni kinga.