15/11/2025
WAAMUZI NYAMAGANA WAONGEZEWA UELEWA KUPITIA MABORESHO YA SHERIA ZA MPIRA WA MIGUU.
Chama cha Mpira wa Miguu Wilaya ya Nyamagana (NDFA) mkoani Mwanza kimetoa mafunzo maalum ya kuongeza uelewa kuhusu maboresho ya Sheria za Mpira wa Miguu kwa waamuzi wa madaraja mbalimbali, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kuboresha uendeshaji wa mchezo huo katika Wilaya ya Nyamagana.
Mafunzo hayo yalifanyika Ijumaa, Novemba 14, 2025 katika Ukumbi wa Mikutano wa Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana, Mkolani – Mwanza, na yaliongozwa na Mkufunzi wa Waamuzi wa Mkoa wa Mwanza, Alfed Lizwa.
Akizungumza wakati wa kumkaribisha mgeni rasmi, Mwenyekiti wa Chama cha Soka Nyamagana (NDFA), Said Abdallah “Kizota”, alisema wanafarijika kuona malengo na mikakati waliyoiweka wakati wa kuomba uongozi yakitekelezwa kwa vitendo.
“Tunawashukuru wadau wote wanaotushika mkono katika kutimiza jukumu hili. Sio kazi rahisi, lakini kwa umoja wetu tumefanikiwa kufanya jambo ambalo wengine walishindwa. Tumekuwa wilaya ya kwanza kutoa mafunzo haya kwa waamuzi wetu ili wawe hodari, makini na wafuate sheria ipasavyo uwanjani,” alisema Kizota.
Akifungua rasmi mafunzo hayo, Katibu Tawala wa Wilaya ya Nyamagana (DAS), Thomas James Salala, alisema Wilaya imejipanga kuendelea kuuwezesha mchezo wa mpira wa miguu ili mafanikio yaonekane kwa matokeo chanya.
Amewaasa waamuzi kujiendeleza na kufuatilia mabadiliko ya sheria mpya za soka ambazo zimefanyiwa maboresho duniani kote kulingana na mahitaji ya sasa ya mchezo huo.
Kwa upande wake, Mkufunzi Alfed Lizwa alisema amefurahishwa na mwitikio wa waamuzi waliojitokeza na kwamba hatua hiyo itaongeza ubora wa usimamizi wa mechi katika mashindano mbalimbali ya wilaya na mkoa.
Naye Makamu Mwenyekiti wa NDFA na Mratibu wa Warsha hiyo, Oscar Kapinga, alisema chama kitaendelea kuratibu mafunzo k**a hayo si kwa waamuzi pekee, bali pia kwa makundi mengine yanayohusika na usimamizi wa mchezo wa mpira wa miguu katika Wilaya ya Nyamagana, ili kuongeza ufanisi na kuleta maendeleo.