18/12/2021
*DC NJOMBE APONGEZA KUKAMILIKA KWA KASI UJENZI DARASA LA UVIKO 19 SHULE YA SEKONDARI UTALINGOLO,
ASEMA NI NAMBA MOJA WILAYA YA NJOMBE.*
*Na Maiko Luoga Njombe*
TR 15.12.2021
Mkuu wa wilaya ya Njombe Mhe, Kissa Gwakisa amepongeza kasi ya ujenzi na ukamilishaji wa chumba cha darasa kilichojengwa kwa fedha za mapambano dhidi ya UVIKO 19 lililopo katika shule ya Sekondari Utalingolo mjini Njombe, akisema darasa hilo ni namba moja wilayani humo.
Mhe, Gwakisa amesema hayo Disemba 15/2021 alipofanya ziara ya kutembelea shule ya sekondari kata ya Utalingolo, kisha kufanya mkutano na wananchi wa kata hiyo akisikiliza kero zao na kuzitafutia ufumbuzi.
“Leo ni Tarehe ya mwisho kukamilisha ujenzi wa madarasa haya ya fedha za UVIKO 19, nawapongeza Viongozi na wananchi wa kata ya Utalingolo mkiongozwa na diwani wenu Mhe, Erasto Mpete kwa kufanikisha ukamilishaji wa darasa hili kwa wakati, ninyi mmekuwa namba moja katika wilaya ya Njombe” Mhe, Kissa Gwakisa.
Diwani wa Kata ya Utalingolo na makamu Mwenyekiti wa Halmashauri ya mji wa Njombe Mhe, Erasto Mpete amesema, darasa hilo limetumia fedha ya UVIKO 19 kiasi cha shilingi milioni ishirini iliyotolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe, Samia Suluhu Hassan.
“Tunamshukuru Mhe, Rais Mama Samia Suluhu Hassan kwa kutuletea fedha hii ambayo imefanikisha kukamilisha jengo hili, pia tunaendelea na ujenzi wa majengo mengine hapa shuleni ikiwemo maabara kwa kutumia fedha za serikali na nguvu za wananchi” Mhe, Erasto Mpete.
Mkuu wa wilaya ya Njombe aliahidi kutoa Kompyuta moja na Printa katika shule ya Sekondari Utalingolo ili kurahisisha utendaji kazi kwa walimu na wanafunzi, huku akipongeza juhudi za Mbunge wa Njombe Mjini Mhe, Deo Mwanyika na Diwani wa Kata ya Utalingolo Mhe, Erasto Mpete za kuchangia shughuli za maendeleo ikiwemo kutoa fedha zao kufanikisha kazi hizo.
“Nimeambiwa hapa kuwa Mhe, Deo Mwanyika Mbunge wa Jimbo la Njombe mjini pamoja na kuchangia kazi za maendeleo, ametoa saruji mifuko 50 kwa kila kijiji cha Kata hii ya Utalingolo, licha ya kwamba hayupo hapa leo naomba nimpongeze sana yeye pamoja na diwani wenu hawa ni viongozi wa kuigwa” alieleza Mhe, Kissa Gwakisa.
Baadhi ya wananchi wa kata ya Utalingolo walioshiriki mkutano huo walimweleza mkuu wa wilaya ya Njombe changamoto ya mlipuko wa bei ya mbolea wakisema, watashindwa kuzalisha mazao katika msimu huu wa kilimo, jambo ambalo Mkuu huyo wa wilaya ya Njombe amesema, Serikali inaendelea kutafuta namna ya kuimaliza kero hiyo.