21/04/2026
Mkongwe wa sinema za Bollywood, Aamir Khan, amewashangaza mashabiki zake baada ya kushea siri nzito kuhusu ndoa yake ya kwanza na Reena Dutta. Katika mahojiano na podikasti ya Raj Shamani, Aamir amesimulia jinsi walivyofunga pingu za maisha kwa siri kubwa na walitumia gharama nafuu.
Aamir alieleza kuwa mapenzi yake kwa Reena yalikuwa ya moto moto kiasi kwamba hakutaka kupoteza muda baada ya kufikisha umri wa kisheria wa kuoa. โTulioana siku ileile ilipowezekana kisheria,โ alisema Aamir. Alitimiza umri wa miaka 21 mnamo Machi 1986 na alifunga ndoa Aprili 18, 1986, akiwa na Reena aliyekuwa na umri wa miaka 19 wakati huo.
Tofauti na harusi za kifahari za mastaa wa sasa, ndoa ya Aamir ilikuwa ya kipekee. Alieleza kuwa walipanda basi namba 211 kuelekea ofisi ya msajili wa ndoa. Gharama nzima ya sherehe hiyo, ikiwemo ada ya usajili na nauli, haikuzidi Rupia 10 za Kihindi.
Licha ya kuwa mke na mume, wawili hao walilazimika kuishi maisha ya siri kwa muda wa miaka miwili. Walichukua uamuzi huo ili kulinda kipaji cha Aamir kilichokuwa kikichipukia na kuepuka migogoro ya kifamilia kutokana na tofauti zao za kidini (Aamir akiwa Muislamu na Reena akiwa Mhindu). Kila mmoja alirudi kuishi kwa wazazi wake kana kwamba hakuna kilichotokea, huku marafiki wachache tu waliokuwa mashahidi ndio wakijua siri hiyo.
Ingawa safari yao ya ndoa ilifikia tamati mwaka 2002 baada ya miaka 16, Aamir amesisitiza kuwa Reena bado ni nguzo muhimu katika maisha yake. Alieleza kuwa heshima na urafiki walionao leo unatokana na msingi imara wa upendo walioujenga tangu wakiwa vijana wadogo wasio na kitu.