09/05/2026
Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Edward Mpogolo, amewataka wazazi na walezi kushiriki kikamilifu katika malezi na maendeleo ya elimu ya watoto wao kwa kuhudhuria vikao vya shule na kushirikiana na walimu kufuatilia maendeleo ya watoto hao.
Akizungumza katika Shule ya Zawadi iliyopo Tabata, jijini Dar es Salaam, Mpogolo amesema mafanikio ya mtoto yanategemea ushirikiano wa pande tatu ambazo ni Serikali, wazazi pamoja na jamii, na wanafunzi wenyewe.
Amesema Serikali ina jukumu la kuboresha miundombinu na kuhakikisha mazingira bora ya kufundishia na kujifunzia kupitia walimu, huku wazazi na jamii wakipaswa kusimamia malezi na kufuatilia mwenendo wa watoto wao. Aidha, wanafunzi wanapaswa kuwa na nidhamu, kuzingatia maadili mema na kuongeza bidii katika masomo yao.
“Tunapozungumzia mafanikio ya mtoto lazima tuzungumzie maeneo matatu makubwa. Serikali ina wajibu wake kupitia walimu, wazazi wana wajibu wao, na wanafunzi nao wanapaswa kuwa na nidhamu na bidii,” amesema Mpogolo.
Aidha, amesema changamoto kubwa inayojitokeza katika shule nyingi za serikali ni mwitikio mdogo wa wazazi wanapoitwa kuhudhuria vikao vya shule, tofauti na ilivyo katika shule binafsi ambapo wazazi wengi hujitokeza kwa wingi kufuatilia maendeleo ya watoto wao.
Mpogolo amesema baadhi ya wazazi huwatuma ndugu, wafanyakazi wa nyumbani au hata madereva wa bodaboda kuhudhuria vikao hivyo kwa niaba yao, jambo ambalo linaathiri mafanikio ya kitaaluma ya mwanafunzi kwa kuwa ushirikiano muhimu kati ya mzazi, mwalimu na mwanafunzi haukamiliki.
“Hivyo ushirikiano wa karibu kati ya wazazi, walimu na wanafunzi ni muhimu sana katika kuhakikisha mtoto anafanya vizuri kitaaluma na kimaadili,” ameongeza.
Amesema Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam imedhamiria kuimarisha ushiriki wa viongozi katika vikao vya wazazi ili kuongeza hamasa ya kufuatilia maendeleo ya wanafunzi.
“Mimi mwenyewe nitafika katika shule zitakazokuwa na vikao vya wazazi ili tuzungumzie maendeleo ya watoto wetu na namna ya kuboresha ufaulu wao,” amesema Mpogolo.