23/06/2026
Serikali imeendelea kuimarisha usimamizi wa ajira za wageni nchini kwa lengo la kuhakikisha ajira hizo zinatolewa kwa kuzingatia sheria na wageni hao wanaoajiriwa wanamiliki vibali halali.
Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano Dkt. Evaline Munisi amesema hayo Juni 23, 2026 Bungeni, Jijini Dodoma wakati akijibu swali la Mheshimiwa John John Nchimbi, Mbunge wa Nyasa, ambaye amehoji Je, nini kauli ya Serikali juu ya Wataalam wa kigeni wanaokaa muda mchache na kupatiwa Business Visa ambayo haitambuliwi na Idara ya Kazi.
Dkt. Munisi amesema kuwa kwa mujibu wa Sheria ya Usimamizi wa Ajira za Wageni, Sura ya 436, vibali vya kazi hutolewa kwa raia wa kigeni wenye mahusiano ya ajira na kampuni au taasisi zinazowaajiri nchini.
Aidha Dkt. Munisi ameonya vitendo vya baadhi ya watu (vishoka) wanaotumia mbinu zisizo halali kuwaleta wageni nchini kwa ajili ya kufanya kazi kinyume cha taratibu, pamoja na kuwawezesha kuendelea kufanya kazi baada ya mikataba yao kuisha kwa kuwatoa nje ya nchi na kurejea tena kwa kutumia pasi nyingine za kuingia nchini. Ameongeza kuwa, Serikali haitasita kuchukua hatua kali za kisheria dhidi ya mtu yeyote au taasisi itakayobainika kukiuka sheria na taratibu za ajira za wageni.