31/08/2026
Baraza la Madiwani la Halmashauri ya Wilaya ya Kaliua mkoani Tabora limewaonya watumishi wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) wilayani humo dhidi ya kutumia lugha zisizo na staha wanapowahudumia wananchi wanaokwenda kufuatilia vitambulisho vya Taifa.
Akizungumza katika kikao cha Baraza la Madiwani, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Kaliua, Anastazia Bebete, amesema baadhi ya wananchi wamekuwa wakilalamikia namna wanavyopokelewa na kuhudumiwa katika ofisi za NIDA, hali ambayo amesema inaweza kudhoofisha zoezi la usajili na ugawaji wa vitambulisho vya Taifa.
Amesema badala ya watumishi kutumia lugha zisizo na staha, wanapaswa kuwaelimisha wananchi na kutatua changamoto zao kwa kuzingatia misingi ya utoaji wa huduma bora.
Kwa upande wake, Katibu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Kaliua, Eliud Shemauya, amesema changamoto nyingine inayowakabili wananchi ni kutozwa fedha wanapokwenda kubadilisha taarifa zao, licha ya zoezi hilo kuwa linapaswa kutolewa bila malipo, jambo ambalo amesema limekuwa likileta sintofahamu.
Wakichangia hoja hiyo, baadhi ya madiwani akiwemo Abdallah Hamisi wa Kata ya Kazaroh, Selina Manamba wa Kata ya Kamsekwa na Sadick Kallah wa Kata ya Ugunga, wameomba zoezi la usajili na utoaji wa vitambulisho liendelee kuwafikia wananchi katika maeneo yao ili kupunguza gharama za kusafiri umbali mrefu kufuata huduma hiyo katika makao makuu ya wilaya.
Awali, akisoma taarifa ya utekelezaji wa zoezi la usajili na utoaji wa vitambulisho vya Taifa kwa kipindi cha robo ya nne ya mwaka wa fedha 2025/2026, Afisa kutoka NIDA Wilaya ya Kaliua, Khamisi Serenge, amesema mamlaka hiyo imefanikiwa kusajili wananchi 7,872, kati ya lengo la wananchi 7,839, baada ya kuwafuata wananchi katika kata za Ichemba, Igwisi, Kanoge, Mwongozo, Nhwande na Silambo.
Hata hivyo, amesema zoezi la ugawaji wa vitambulisho bado linakabiliwa na changamoto, ambapo kati ya vitambulisho 6,779 vilivyopelekwa katika kata hizo ili wananchi wavichukue, ni vitambulisho 1,204 pekee vilivyochukuliwa na wahusika.
Aidha, Serenge amesema ucheleweshwaji wa upatikanaji wa rasilimali fedha umekuwa ukisababisha kuchelewa kwa utekelezaji wa zoezi la usajili kwa kuwafuata wananchi.