18/08/2025
Katika kuelekea uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika October 29 mwaka huu, Waandishi wa habari nchini wametakiwa kufanya shughuli zao kwa kuzingatia maadili ya taaluma hiyo.
Aidha wametakiwa kutoa elimu kwa wananchi ili waweze kupata taarifa sahihi na kwa wakati sisizokuwa na upendeleo wowote, zisizokweza utu wa mtu ili kufanya uchaguzi huo kuwa wa haki usalama na amani kwa maslahi ya Taifa.
Kauli hiyo imetolewa leo Agost 16, 2025 na mkuu wa wilaya ya Longido Salum Kali kwa niaba ya mkuu wa mkoa wa Arusha Kenan Kihongosi alipokua akifungua mkutano wa wadau wa sekta ya habari na utangazaji kuelekea uchaguzi mkuu uliofanyika katika ukumbi wa kimataifa wa AICC jijini Arusha.
Awali Kaimu Mkurugenzi wa idara ya Habari maelezo Rodney Mbuya amesema kutokana na sekta ya habari kubeba dhamana kubwa ya kiusalama nchini ndio maana idara ya habari maelezo imeandaa mkutano huo kwa lengo la kubadilisha mawazo ili wananchi waweze kupata taarifa za msingi, sahihi na kwa wakati na zisizo na upendeleo.
Akitoa mada kuhusu mwongozo wa waandishi wa habari katika uandishi wa habari za uchaguzi Mhadhiri kutoka chuo kikuu cha Dar es salaam (UDSM) Dkt. Egbert Mkoko amesema mwandishi wa habari anayepaswa kuripoti habari za uchaguzi ni yule aliyethibitishwa na bodi ya ithibati (JAB)
Akiwasilisha mada kuhusu kanuni za utangazaji wa uchaguzi kwa vyama vya siasa za mwaka 2020 Meneja wa Huduma za Utangazaji wa TCRA, Mhandisi Andrew Kisaka, amesema vyombo vya habari vinapaswa kuweka mizania kwa vyama vya siasa ili kuepuka kuegemea upande wowote.
Akiwasilisha mada kuhusu wajibu wa waandishi wa habari na Jeshi la Polisi katika kulinda usalama kuelekea uchaguzi mkuu Msemaji wa Jeshi la Polisi nchini DCP David Misime amesema waandishi wa habari na Jeshi la Polisi wana wajibu wa kulinda amani kabla wakati na baada ya uchaguzi.
"Waandi wa habari na Keshi la Polisi tuna jukumu kubwa la kulinda usalama wa nchi, Jeshi la Polisi likishirikiana vyema na waandishi wa habari nchi itabaki salama hivyo mtumie kalamu zenu vizuri wakati wa kuripoti habari za uchaguzi" Amesema Misime.
Na Salimu Omari Ally