03/03/2026
Kupitia taarifa rasmi iliyotolewa leo Machi 3, 2026 jijini Dodoma, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki imesema inafuatilia kwa karibu mwenendo wa hali ya usalama katika nchi za Mashariki ya Kati.
Serikali imewashauri Watanzania waliopo au wanaotarajia kusafiri kwenda katika mataifa ikiwemo Bahrain, Israel, Kuwait, Qatar, Falme za Kiarabu (UAE) na Oman, kuchukua tahadhari za ziada kutokana na mazingira ya sasa ya kiusalama.
Miongoni mwa maelekezo yaliyotolewa ni:
Kuepuka safari zisizo za lazima kwenda au kutoka katika eneo hilo kwa kipindi hiki.
Kubaki katika makazi au maeneo salama yanayopendekezwa.
Kufuata maelekezo ya mamlaka za maeneo husika.
Kuepuka maeneo yenye shughuli za kijeshi au kiusalama.
Kutumia njia rasmi za mawasiliano kwa taarifa na msaada.
Kuhifadhi pasipoti na nyaraka muhimu sehemu salama.
Aidha, Serikali imewataka Watanzania walioko katika ukanda huo kujisajili kupitia mfumo maalum wa usajili wa diaspora kwa ajili ya uratibu na ufuatiliaji wa karibu endapo dharura itatokea.
Kwa dharura au maelezo zaidi, raia wametakiwa kuwasiliana na balozi za Tanzania zilizo karibu nao au kufuatilia taarifa rasmi kutoka serikalini.
ANCHOR OUTRO:
Serikali imehimiza utulivu na uangalifu, huku ikiendelea kufuatilia kwa karibu hali ya usalama katika ukanda wa Mashariki ya Kati.
Hiyo ni taarifa kwa sasa.