12/08/2026
BENKI ya Taifa ya Biashara (NBC) imesisitiza dhamira yake ya kuendelea kuunga mkono juhudi za Serikali na wadau mbalimbali katika kukuza matumizi ya nishati safi ya kupikia, kuhifadhi mazingira, kukuza utalii na kuendeleza ubunifu wa vijana.
Dhamira hiyo ilibainishwa jana na Mkurugenzi Mtendaji wa NBC, Theobald Sabi, wakati wa hafla maalum ya mnada wa sanaa za picha iliyoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika Hoteli ya Kwanza, Kizimkazi, Zanzibar.
Hafla hiyo iliandaliwa na Mwanamke Initiative Foundation (MIF) kwa kushirikiana na kampuni ya ubunifu ya Waba Group, ikiwa na lengo la kutumia sanaa ya upigaji picha kuhamasisha uhifadhi wa mazingira, nishati safi ya kupikia na utalii.
Picha zilizopigwa katika maeneo mbalimbali ya Zanzibar zilionesha mandhari, utamaduni, maisha ya jamii, utalii na urithi wa asili wa visiwa hivyo.
Akizungumza katika hafla hiyo, Rais Samia aliwataka wadau wa sanaa ya upigaji picha, hususan vijana, kutumia ubunifu wao katika kuitangaza Tanzania na vivutio vyake vya utalii.
Alisema sekta hiyo ina fursa kubwa za kibiashara na inaweza kuwa chanzo cha ajira na kipato kwa vijana.
Rais Samia pia alieleza kuvutiwa na baadhi ya picha zilizowasilishwa, zikiwemo za pomboo chini ya bahari, wanawake wakilima mwani na mandhari mbalimbali za Zanzibar.
Alisema kazi hizo zinaweza kutumika kuitangaza Tanzania, utamaduni wake na vivutio vyake katika soko la ndani na kimataifa.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Mwanamke Initiative Foundation, Wanu Hafidh Ameir, alisema fedha zitakazopatikana kupitia mnada huo zitaelekezwa katika kuunga mkono jitihada za kukuza matumizi ya nishati safi ya kupikia na kupunguza utegemezi wa nishati zinazochangia ukataji wa misitu.
Akizungumzia nafasi ya NBC katika agenda ya nishati safi ya kupikia, Sabi alisema benki hiyo iko tayari kushirikiana na wadau mbalimbali kuwezesha mnyororo mzima wa nishati hiyo, kuanzia uzalishaji hadi matumizi.
Katika hafla hiyo, NBC ilitunukiwa tuzo maalum na Rais Samia kwa kutambua mchango wake katika kufanikisha tukio hilo na kuunga mkono ajenda ya maendeleo endelevu, ikiwemo nishati safi ya kupikia na uhifadhi wa mazingira.