Zanzibarleo Online

Zanzibarleo Online Pata habari za uhakika na kuaminika kutoka Gazeti namba 1 visiwani Zanzibar na Tanzania kwa ujumla.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi, anatarajiwa kuwa mgeni rasmi kwenye ufung...
27/06/2025

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi, anatarajiwa kuwa mgeni rasmi kwenye ufunguzi wa kongamano la siku mbili, litakalowashirikisha viongozi wa elimu ya juu barani Afrika.

Akitoa taarifa kwa vyombo vya habari, Makamu wa Rais wa taasisi ya QS ya Uingereza, Ben Sowter, alisema kongamano hilo litafanyika Julai 3 hadi 4 mwaka huu katika ukumbi wa hoteli ya Golden Tulip.

Makamu huyo alisema kongamano la viongozi wa elimu ya juu barani Afrika linalenga kujadili namna ya kutumia elimu ya juu k**a kichocheo cha mageuzi barani humo.

Alibainisha kuwa kongamano hilo pamoja na mambo mengine litajadili mbinu zitakazosaidia bara la Afrika kuvipatia vizazi vijavyo maarifa, ujuzi na fursa zitakazowawezesha kuchangia kikamilifu katika ukuaji wa uchumi, uvumbuzi na maendeleo ya kijamii.

Alisema kuwa tukio hilo la kihistoria, mbali ya kuhudhuriwa na viongozi wa vyuo vikuu, pia litawashirikisha watendaji na viongozi wa serikali na sekta ya viwanda.

SERIKALI ya Uganda kupitia Ubalozi wake mjini Tehran, imesema imefanikiwa kuratibu zoezi la kuwaondoa salama raia 42 wa ...
23/06/2025

SERIKALI ya Uganda kupitia Ubalozi wake mjini Tehran, imesema imefanikiwa kuratibu zoezi la kuwaondoa salama raia 42 wa Uganda na wafanyakazi wawili wa kidiplomasia kutoka Jamhuri ya Kiislamu ya Iran hadi Jamhuri ya Uturuki.

Hali hiyo inafuatia kuzuka kwa mapigano kati ya Iran na Israel tangu Juni 13 mwaka huu ambayo yameathiri pakubwa hali ya usalama katika eneo hilo.

“Mchakato wa kuwahamisha watu hao uliongozwa na ubalozi wa Uganda mjini Tehran, chini ya uongozi wa Makao Makuu ya Wizara ya Mambo ya Nje mjini Kampala, na kwa usaidizi mkubwa kutoka Ubalozi wa Uganda mjini Ankara, Uturuki.”

Serikali ya Uganda inasema kuwa kituo cha kuratibu uokoaji wa dharura kilianzishwa kwa haraka nchini Uturuki ili kuwezesha usajili, uratibu na harakati salama za raia wa Uganda.

“Katika onesho la mfano la ushirikiano na mwitikio, Jamhuri ya Uturuki ilikubali ombi la Uganda la kutoa visa wakati wa kuwasili watu walioathirika, kuruhusu usafiri wao wa haraka na kuingia kwa muda katika eneo la Uturuki k**a sehemu ya mchakato wa kuwahamisha”, serikali ya Uganda imesema.

Usafiri wa ardhini kutoka Tehran hadi Uturuki ulipangwa, na kundi la kwanza lilipokelewa kwa mafanikio kwenye mpaka wa Bargarzan Juni 18 mwaka 2025.

Wizara ya Mambo ya Nje ya Uganda imesema wanafunzi 42 wa Uganda na wafanyakazi wawili wa ubalozi kwa sasa wako katika usafiri wa kuelekea Istanbul, ambako wameratibiwa kupanda ndege ya kukodi kurudi nyumbani Uganda.

WANAJESHI saba wa Uganda wameuawa nchini Somalia, katika makabiliano makali ya kudhibiti mji wa Sabiid-Anole kutoka kwa ...
23/06/2025

WANAJESHI saba wa Uganda wameuawa nchini Somalia, katika makabiliano makali ya kudhibiti mji wa Sabiid-Anole kutoka kwa magaidi wa Al Shabab kwenye jimbo la Shabelle.

Jeshi la Uganda, limethibitisha kuuawa kwa wanajeshi hao waliokuwa kwenye kikosi cha Umoja wa Afrika kinachosaidia kurejesha amani nchini Somalia AUSSOM.

Mashambulio ya Al Shabab, yameripotiwa kuongezeka katika miezi ya hivi karibuni, wakati huu Umoja wa Afrika, ukikabiliwa na changamoto ya uhaba wa wanajeshi na fedha za kuendeleza operesheni zake.

Kikosi cha AUSSOM ambacho kina wanajeshi zaidi ya 11,000 kutoka nchi mbalimbali za Afrika, kilichukua nafasi ya ATMIS na mwezi Aprili, kilisema kinahitaji wanajeshi wengine zaidi ya 8,000.

Somalia kwa kipindi kirefu sasa, imeendelea kusumbuliwa na magaidi wa Al Shabab, ambao wamekuwa wakitekeleza mashambulio dhidi ya raia, na maafisa wa serikali, kwa lengo la kuchukua madaraka jijini Mogadishu.

Kuongezeka kwa mashambulizi ya hivi karibuni ya Al Shabaab yamezua hofu ya kuibuka tena kwa makundi ya itikadi kali katika taifa hilo la Pembe ya Afrika, hasa wakati huu kikosi cha AUSSOM kilichochukua nafasi ya kile cha ATMIS kikipambana na ukosefu wa askari wa kutosha pamoja na upungufu wa fedha.

KATIKA kuadhimisha wiki ya Utumishi wa Umma mwaka huu, Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF), umeweka mkazo katika kueli...
23/06/2025

KATIKA kuadhimisha wiki ya Utumishi wa Umma mwaka huu, Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF), umeweka mkazo katika kuelimisha umma kuhusu magonjwa yasiyoambukiza na kuhimiza matumizi ya mifumo ya kisasa ya kidijitali katika upatikanaji wa huduma zake.

Akizungumza kwenye viwanja vya maadhimisho hayo jijini Dodoma, Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano wa NHIF, James Mlowe, alisema ongezeko la magonjwa yasiyoambukiza k**a kisukari, shinikizo la damu na magonjwa ya moyo limeendelea kuwa changamoto kubwa kwa sekta ya afya.

“Kwa sasa, zaidi ya asilimia 60 ya gharama zote za matibabu tunayolipa kila mwaka zinahusiana na magonjwa yasiyoambukiza, kwa mfano, mwaka uliopita NHIF ilitumia takribani shilingi bilioni 700 kwa ajili ya huduma kwa wanachama wake”, alisema.

Mlowe alisisitiza umuhimu wa elimu kwa jamii kuhusu namna ya kujikinga na maradhi hayo, akisema juhudi hizo zitasaidia kupunguza gharama kubwa za matibabu na kuruhusu fedha kuelekezwa katika kuboresha huduma nyingine za afya.

Aidha, alisema NHIF imeongeza kasi ya mageuzi ya kidijitali kupitia mfumo wa "NHIF Jihudumie", unaowezesha wanachama kujihudumia kupitia simu za mkononi.

“Mwanachama sasa anaweza kutumia kadi ya kidigitali kupata huduma katika vituo zaidi ya 10,000 vilivyosajiliwa na NHIF nchi nzima,Hii ni hatua kubwa katika kupunguza msongamano na kuimarisha ufanisi wa huduma,” aliongeza.

Soma zaidi, tembelea: 𝒘𝒘𝒘.𝒛𝒂𝒏𝒛𝒊𝒃𝒂𝒓𝒍𝒆𝒐.𝒄𝒐.𝒕𝒛

Address

Maisara
Zanzibar

Alerts

Be the first to know and let us send you an email when Zanzibarleo Online posts news and promotions. Your email address will not be used for any other purpose, and you can unsubscribe at any time.

Contact The Business

Send a message to Zanzibarleo Online:

Share