23/06/2025
KATIKA kuadhimisha wiki ya Utumishi wa Umma mwaka huu, Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF), umeweka mkazo katika kuelimisha umma kuhusu magonjwa yasiyoambukiza na kuhimiza matumizi ya mifumo ya kisasa ya kidijitali katika upatikanaji wa huduma zake.
Akizungumza kwenye viwanja vya maadhimisho hayo jijini Dodoma, Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano wa NHIF, James Mlowe, alisema ongezeko la magonjwa yasiyoambukiza k**a kisukari, shinikizo la damu na magonjwa ya moyo limeendelea kuwa changamoto kubwa kwa sekta ya afya.
“Kwa sasa, zaidi ya asilimia 60 ya gharama zote za matibabu tunayolipa kila mwaka zinahusiana na magonjwa yasiyoambukiza, kwa mfano, mwaka uliopita NHIF ilitumia takribani shilingi bilioni 700 kwa ajili ya huduma kwa wanachama wake”, alisema.
Mlowe alisisitiza umuhimu wa elimu kwa jamii kuhusu namna ya kujikinga na maradhi hayo, akisema juhudi hizo zitasaidia kupunguza gharama kubwa za matibabu na kuruhusu fedha kuelekezwa katika kuboresha huduma nyingine za afya.
Aidha, alisema NHIF imeongeza kasi ya mageuzi ya kidijitali kupitia mfumo wa "NHIF Jihudumie", unaowezesha wanachama kujihudumia kupitia simu za mkononi.
“Mwanachama sasa anaweza kutumia kadi ya kidigitali kupata huduma katika vituo zaidi ya 10,000 vilivyosajiliwa na NHIF nchi nzima,Hii ni hatua kubwa katika kupunguza msongamano na kuimarisha ufanisi wa huduma,” aliongeza.
Soma zaidi, tembelea: 𝒘𝒘𝒘.𝒛𝒂𝒏𝒛𝒊𝒃𝒂𝒓𝒍𝒆𝒐.𝒄𝒐.𝒕𝒛